Monday, January 14, 2013

BARUA KWA 2013

Na Chris Wambui

Mpendwa 2013, Hujambo mwaka mpya? Niruhusu nikuite mwaka mpya kwa sababu mimi ni Mkenya na ni kawaida yetu kusalimiana salamu za mwaka mpya hadi Aprili.

Rafiki yangu kama ujuavyo nilikuwa nimekungoja kwa hamu na ghamu ufike. Wakenya wengi tulisherekea kuchukua usukani kwako kutoka kwa mwenzako 2012. Pombe mingi ilimwagwa tumboni za watu. Mbuzi, ngombe, kuku na hata punda walipoteza uhai. Hela tulitumia bila fikra na vyoo vilijazwa, kwa ajili yako wewe, ili tukusherehekee. Lakini hata baada ya hayo yote, kwa nini ulitusaliti?

Wiki mbili hazijaisha na Wakenya wengi wamepoteza uhai. Tuliona watu hamsini na saba wakifa kwa muda wa siku mbili tu za mwaka huu kwa ajili ya ajali.

Rafiki yangu 2013, ulipoingia, hata kabla ubugie chumvi kawe, tulishuhudia mauaji eneo la Tana. Tumeshuhudia mauaji mtaa wa Mathare na uharibifu wa mali. Hata kabla tukujue kiasi, tumeona vile watu hawana soni kujifanya wana polisi. La kukera zaidi ni kwamba jua limetua kwa vipara zetu na hela zimeadimika kama mayai ya nguruwe.

Mpendwa 2013, kwa niaba ya marafiki zangu na jamaa, nimekuandikia kukujulisha tumechoshwa na bahati zako mbaya. Tafadhali usijiharibie jina kwa kutoleta heri njema. Badilisha mkondo wa mwia uliobaki tafadhali, ndiposa tukusherehekee muda wako wa mamlaka utakapoisha.

Wako mwaminifu,Chris msikitivu...

No comments:

Post a Comment

your comment, your voice...

Search site.